Shafi Adam Shafi aliyeadika Kasri ya Mwinyi Fuad na Kuli, anainua kiwango na hadhi ya fasihi ya Kiswahili katika riwaya hii ya Vute N’kuvute.
Kwanza, kuna ndoa ya Yasmin, mtoto wa kihindi kwa Bwana Raza, mzee sawa na babu yake. Yasmin anafukuzwa na wazee wake kwa kumwacha Raza. Katika upweke wake, anasitiriwa na Mwajuma, shoga yake anayeishi ili kustarehe katika dansa, taarab na pegi za vikali. Yasmin anaingizwa uswahilini. Kuna wivu unaopelekea kifo cha Shibab, mume wa pili wa Yasmin. Kuna Denge, Yasmin anampenda lakini hapendeki. Kwa Denge ni mapambano na ukoloni tu na makachero wake. Hii ni vuta n’ kuvute ambayo sharti yeye na wenzake waishinde.
Kuna Bukheti. Kaja Unguja kumfuata Yasmin. Yasmin hakubali kuolewa na Bukheti kama hatashiriki katika kumtorosha Denge kutoka jela ya mkoloni alikofungwa. Mapenzi na mapinduzi. Yasmin naye kajitosa katika vuta n'kuvute hii ya kumpenda Denge na ya siasa. Kutoka katika kungojea wanaume waamue sudi yake; yeye naye sasa ni mtenda, si mtendewa tu.
Riwaya hii ilipata tuzo kwa mswada bora wa riwaya ya Kiswahili hata kabla ya kuchapishwa, kwenye Tamasha la Vitabu, Dar es Salaam kwa mwaka 1998. Hakiwekeki chini kitabu hiki; kitakuvuta na utakubali kikuvute. Ni kitabu kitakachozungumzwa kwa muda mrefu.